Tuesday, February 7, 2012

HATULIPANI TENA POSHO....NDUGAI

 
Ndugu zangu,

Gazeti Uhuru  jana Jumanne limebeba habari hiyo kwenye ukurasa wa kwanza.
Mwandishi Lilian Timbuka akiripoti kutoka Dodoma  anamnukuu Naibu Spika wa Bunge Job Ndugai akitamka; ” Nyongeza ya  posho ya vikao vya bunge sasa haitalipwa mpaka hapo Ofisi ya Rais, Ikulu, itakapotamka vinginevyo. Kwa kuwa  Rais ndiye mwenye  mamlaka ya kuidhinisha vibali vya nyongeza za malipo kwa wabunge, ikiwemo posho na hajatoa kibali, hivyo haina haja ya kuendeleza mjadala kuhusu hoja hiyo”- Job Ndugai, Uhuru, Jumanne, Februari 7, 2012.


Nionavyo:
Iko haja , kama nchi, kuendeleza mjadala huu wa posho kwa vile suluhisho la kudumu halijapatikana. Tuendelee kujadili  maana  posho za waheshimiwa sasa ni moja ya kero za wananchi.  Tumefika mahali tuamue, kama taifa, tunatunga sheria itakayopiga marufuku ya posho za vikao kwa  viongozi wakiwamo wabunge na watumishi wa Serikalini na Mashirika ya umma.

Kuendelea na utamaduni wa kulipana posho ni kundekeza  utamaduni wa hovyo hovyo.  Kwanini Mbunge au Mtumishi Serikalini alipwe posho ya kikao  wakati yuko kazini?  Kwanini mtumishi akikaa ofisini kwake Wizarani halipwi posho bali mshahara na anapohamishia kazi ya Wizara  Ubungo Plaza analipwa posho ya kukaa na kufanya kazi hiyo hiyo anayolipwa mshahara kila mwezi? Huu ni  ufujaji wa fedha za wananchi. Ni ufisadi.

Hatukubali kauli za kuwa Wabunge wetu wana hali ngumu. Eti tunaambiwa  posho wanazopata zinawasaidia katika kuwasaidia wananchi majimboni mwao. Hivi ni wapi panaposema kuwa kazi ya mbunge ni kugawa fedha kwa wananchi wa jimbo lake?  
Eti tunaambiwa pia, kuwa Mbunge inapofika mwisho wa mwezi anakosa hata fedha za mafuta ya gari yake!  Hapa kwanza inategema anatumia gari ya aina gani na anaitumiaje. Na hakika, mbunge anayekosa hela ya mafuta ya gari yake yumkini anayeshindwa kusimamia mapato na matumizi yake kiasi cha kuishiwa hata fedha ya kujaza mafuta ya gari yake, basi, atakuwa amepungikiwa hata na sifa za uongozi.

Ndugu zangu,

Matatizo mengi ya kiuchumi ya wabunge wetu ni ya kujitakia. Na matatizo mengi ya kiuchumi ya wananchi walio wengi yanachangiwa sana  na baadhi ya viongozi tuliowapa dhamana  kuendekeza ubinafsi.  Tuna viongozi leo wanaonyesha kuwa mbali na wananchi na kukosa mguso wa hali halisi za wananchi. Wamesimama  juu kwenye Ivory towers wakati wananchi nchi wakitahabika.  Wabunge wetu kuendelea kung’ang’ania nyongeza ya posho katika wakati huu mgumu kwa wengi ni kielelezo cha wao kukosa mguso na hali halisi za wananchi wanaowawakilisha.

Na kuna waheshimiwa wanaosema, kuwa hawakuchaguliwa kuwa wabunge ili wawe masikini. Nasi tunasema,  tumewachagua kuwa wabunge ili waende wakatutumikie  wananchi na si matumbo yao.

Ndugu zangu,

Yawezekana kabisa unavyosoma  makala hii kuna mama MTanzania anayejifungua akiwa  amelala sakafuni, au kuna mtoto wa KiTanzania anayekufa kwa malaria kwa vile zahati haina dawa. Ndio hali halisi. Huu ni wakati kwa viongozi wetu kuacha kuendekeza ubinafsi. Sakata la wabunge kuongezewa posho ni kielelezo cha ubinafsi.

Viongozi wakiwamo Wabunge waanze sasa kuwafikiria wananchi ambao wengi wako katika hali mbaya
kiuchumi. Ni wananchi hawa ambao miongoni mwao kuna wakulima. Ni wakulima hawa ambao posho ya laki mbili kwa siku kwa mbunge ingetosha kwa mkulima huyu kununua mbolea mifuko mitatu ya kila hamsini kwa mfuko. Ni mbolea ya kupandia na kukuzuia kwa ekari moja. Tujiulize; tuko sasa kwenye ”

Kilimo Kwanza au Wabunge Kwanza?” Na kuna kisa cha ndani ya kitabu cha ’ Animal Farm’- "Shamba la Wanyama". Katika kitabu hicho;Mwandishi George Orwell anatupa taswira ya jamii tunayoishi. Mwandishi anaandika juu ya wanyama waliochoshwa na hali ya kunyanyasika kama watumwa , adha na maovu ya kila namna waliofanyiwa na Bwana Jones, mmiliki wa shamba na binadamu wengine.

Wanyama waliamua kufanya maasi. Walifanikiwa na kuwaondoa shambani wanadamu wote. Walianza kujitawala. Hali ilibadilika ghafla. Napolioni ambaye ndiye alikuwa Nguruwe Mkuu, alianza udikteta. Napolionibalifanya matendo ya uovu. Alijipendelea na aliwapendelea nguruwe wenzake. Shambani humub tunakutana na wanyama wa kila aina, mathalan, kuna kondoo wapumbavu, na hata mbwa wenye hasira fupi za mara kwa mara. Kuna kuku na mabata wenye hofu kubwa wakati wote.



Inaonyesha pia ni jinsi gani, baadhi yetu wanadamu, mara tu tunapokutana na madaraka, basi, huvimba vichwa na kujiona tuna tofauti kabisa na wengine tulio nao kwenye kundi moja. Tunajibagua kuto ka kwenye kundi kuu na kuunda tabaka letu. Tunalewa madaraka.



Kisa cha "Shamba La Wanyama" kinatukumbusha wajibu wetu. Kwamba siku zote tuwe macho dhidi ya wale wote wenye hulka za kidikteta. Wenye kujipendelea na kutanguliza maslahi yao mbele kuliko ya umma. Wenye kufanya maamuzi bila kutuhusisha wananchi. Bila kusubiri wala kusikiliza maoni yetu. Bila kutujali.

Katika kitabu hiki tunaona pia jinsi wanyama wanavyoshindwa kudhibiti hali iliyoko. Kudhibiti mwelekeo wao. Wanashindwa kufanya hivyo hata kama wanaona kwa macho yao maovu yafanyikayo. Tunaona ni jinsi gani nguruwe wasivyoaminiwa na "ndugu zao". Kwa maana ya wanyama wenzao shambani. Kwamba nguruwe wameachana na dhumuni halisi la kufanya mapinduzi, kupata uhuru wao. Dhumuni la kujitawala. Nao wamegeuka wala rushwa na wasio wakweli kama ilivyo katika mashamba ya jirani. Wamelewa madaraka.

Nguruwe hawa wanajaribu kuficha maovu watendayo kwa wanyama wenzao kwa kuwafanya waamini, kwamba bado wanapigania itikadi na malengo yale yale yaliyowalazimisha wafanye mapinduzi. "Komredi!" alitamka nguruwe kwa sauti kuu.

"Sidhani kama mtaweza kufikiri, kwamba sisi nguruwe tunafanya haya kwa kujali maslahi yetu ikiwemo marupurupu mengine? Kwa kweli wengi wetu (nguruwe) hatupendi maziwa na matunda. Binafsi sipendi.

Tunakunywa maziwa na kula matunda kwa lengo moja tu, kutunza afya zetu. Komredi!, Hii imethibitishwa na wanasayansi, kwamba maziwa na matunda yana vitu muhimu ndani yake. Vitu ambavyo ni muhimu kwa afya ya nguruwe.
Mnajua, sisi nguruwe tunafanya kazi kwa kutumia ubongo. Uongozi na utawala wa shamba hili unatutegemea sisi. Hatulali. Usiku na mchana tuko macho kuyaangalia maslahi yenu. Ni kwa maslahi yenu, ndio maana tunakunywa maziwa na tunakula matunda.

 Je, mnajua kipi kitatokea kama sisi nguruwe tutashindwa kutekeleza wajibu wetu? Jones (mkoloni, kama ukipenda) atarudi tena! Ndio, mkoloni atarudi tena! Komredi, nawaambia ukweli." Alitamka nguruwe kwa sauti ya kushawishi ili aaminike huku akitingisha mkia wake. " Kweli, hivi kuna mmoja wetu anayetaka Jones ( mkoloni) arudi tena? (Animal Farm, Uk. 22)
Maelezo ya hapo juu yanaonesha ni jinsi gani nguruwe kwa kutumia hisia na hofu ya Jones (mkoloni) kurudi tena kama nyenzo ya kuendelea kuwadhibiti wanyama shambani. Kwamba wao ndio wenye kuhenyeka na hivyo basi kustahili upendeleo maalumu katika jamii.



Cha kutisha zaidi, ni ile hali ya wanyama hawa kufikia kuchinjana wenyewe kwa wenyewe kutokana na
kuchanginyiwa na kukata tamaa. ( Rwanda, Kongo) Hii inatuonyesha, kuwa hata yale ambayo kimsingi yalifanywa kwa pamoja kwa nia njema kabisa , mathalan, hili la kudai uhuru wetu kutoka kwa wakoloni, hufikia mahala watu wakachinjana katika kudai haki zao.

Tulipo sasa ni kwa baadhi ya viongozi wetu kuiegeuza nchi yetu kuwa ni gulio la mafisadi. Kwamba kila mwenye uwezo atafute mtaji. Awahi nafasi ya uongozi itakayomsaidia kuingia gulioni. Huko ni mahala pa kufanya biashara , si kuwatumikia wananchi. Kwa bahati mbaya, hata rasilimali zetu wanazipeleka gulioni.
Ili kuinusuru nchi yetu, sote kwa pamoja. Bila kujali itikadi zetu za vyama, tuna lazima ya kulifunga gulio hili. Sasa.

Maggid Mjengwa,

No comments:

Post a Comment